Friday, January 17, 2014

Majina ya wabunge ‘majangili’ Yaanikwa:

 
 
 Utata umeibuka kuhusu wabunge waliotajwa kwenye ripoti ya Kamati ndogo ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira kuwa wanahusika na biashara ya pembe za ndovu.
Wakati Ofisi ya Bunge ikidai kuwa ripoti hiyo haina majina ya wabunge, Mwenyekiti wa kamati hiyo, James Lembeli ameshikilia kuwa majina hayo ni sehemu ya ripoti hiyo ambayo baada ya kuwasilishwa, iliibua mjadala ambao ulisababisha mawaziri wanne kuong’oka.
Gazeti hili limedokezwa kuwa majina ya wabunge hao yalitajwa mbele ya kamati hiyo wakati ikichunguza jinsi Operesheni Tokomeza Ujangili ilivyotekelezwa, baada ya kuwapo kwa malalamiko ya vitendo vya ukatili na utesaji wa raia.
Hata hivyo, kwa mujibu wa taarifa hizo, wabunge hao hawakuitwa mbele ya kamati hiyo kuhojiwa kutokana na kwamba suala hilo halikuwa moja ya hadidu za rejea walizopewa kuzitafutia majawabu.
“Sisi tulimaliza kazi na kuikabidhi Ofisi ya Bunge, ni kweli majina hayo hayamo kwenye ripoti (iliyosomwa bungeni) lakini nilikuwa navyo kwenye viambatanisho na ushahidi wake,” alisema Lembeli jana.
Alipoulizwa sababu za kutokuweka majina ya wabunge hao katika taarifa iliyosomwa bungeni Desemba 20, mwaka jana, mbunge huyo wa Kahama alisema: “Hiyo haikuwa kazi yetu sisi tulikuwa na wajibu wa kueleza yaliyotokana na Operesheni Tokomeza tu, lakini hayo mengine yapo kwenye viambatanisho.”
Ripoti ya kamati ndogo iliweka bayana jinsi watu mbalimbali walivyoteswa na vyombo vya dola wakati wa operesheni hiyo na baada ya mjadala bungeni, Rais Jakaya Kikwete alitengua uteuzi wa mawaziri hao.
Mawaziri wanne walioachishwa ni pamoja na Dk Emmanuel Nchimbi (Mambo ya Ndani), Shamsi Vuai Nahodha (Ulinzi na JKT), Balozi Khamis Kagasheki (Maliasili na Utalii) na Dk Mathayo David (Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi).
Ofisa wa Bunge, ambaye aliomba kuhifadhiwa jina lake alisema taarifa iliyowasilishwa bungeni siku hiyo haikutaja majina ya wabunge hao na kwamba hata kwenye Hansard (taarifa za Bunge), za siku ya mjadala huo suala hilo halimo.
“Wabunge ni kama walifanya makosa, baada ya mwenyekiti (Lembeli) kusema kwamba wabunge wanatajwa kwa ujangili, walipaswa kutumia kanuni maana zipo, kutaka majina yao yatajwe,” alisema ofisa huyo.
Kauli yake iliungwa mkono na Naibu Spika, Job Ndugai ambaye alisema: “Kimsingi kwa mujibu wa taratibu za Bunge, taarifa inayowasilishwa bungeni ndiyo inayosomwa na ni wazi kwa umma, haiwi siri.”
Ndugai alisema katika mazingira hayo, isingekuwa siri kama majina hayo yangetajwa kwenye taarifa ya kamati. posted by http://thesuperonenews.blogspot.com

0 comments:

Post a Comment