Saturday, June 29, 2013

WANYAMA SAFARI YAIVA ENGLAND

WANYAMA

MCHEZAJI wa Kimataifa wa Kenya, Victor Wanyama, anaechezea Klabu ya Scotland, Celtic, yuko mbioni kujiunga na Klabu za BPL, Barclays Premier League baada ya Ofa kadhaa kumiminika za kumnunua.
Hivi Juzi, Ofa ya Southampton ya Dau la Pauni Milioni 12 ilikubaliwa na Klabu ya Celtic lakini Wanyama, mwenye Miaka 21, alishindwa kukubaliana na Southampton kuhusu Maslahi yake binafsi.
Hivi sasa, Klabu iliyopanda Daraja Mwezi Mei na Msimu ujao wa 2013/14 unaoanza Agosti itacheza BPL, Cardiff City imetoa Ofa mpya kwa Celtic baada ya kwanza kugomewa na pia imependekeza Maslahi ambayo yanakubalika na Wanyama.
Wanyama alijiunga na Celtic Mwaka 2011 kwa Dau la Pauni Milioni 1 kutoka Klabu ya Ubelgiji Germinal Beerschot na hivi sasa amebakisha Mkataba wa Mwaka mmoja tu na Celtic ambao ndio Mabingwa wa Scotland.
Celtic wameshakiri kuwa Mkenya huyo ataihama Klabu yao lakini hivi karibuni wamekuwa wakikwaruzana na Wakala wa Wanyama, Ivan Modia.
Modia amekuwa akidai Wanyama amekaa Celtic Miaka miwili bila ya kuongezewa Mshahara na pia Mwaka Jana alikataliwa kujiunga na Queen’s Park Rangers.
Licha ya kukiri Wanyama ataondoka, Meneja wa Celtic, Neil Lennon, pia amekubali kuwa kuondoka kwa Wanyama kutaleta pengo kubwa kwao lakini itabidi wamruhusu ikiwa itakuja Ofa inayolingana na thamani ya Mchezaji huyo. 

0 comments:

Post a Comment